Dar es
Salaam. Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji
Joseph Warioba amewashangaa makada wanaojinadi kuwa ni wasafi na
waadilifu, akisema sifa hizo zinatakiwa zitolewe na jamii.
Jaji
Warioba, mmoja wa watu ambao wamekuwa wakikemea masuala ya ukiukwaji wa
maadili, pia amesema hatamuunga mkono mgombea ambaye anakiuka maadili ya
uongozi.
Tayari
makada 37 wamejitokeza kuomba ridhaa ya wana-CCM kugombea urais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na wengi wao wamekuwa wakijinadi kuwa
ni wasafi na waadilifu na kuwataka wanachama kutowapitisha watu wenye
harufu ya ufisadi na wasio waadilifu.
Lakini Jaji Warioba alisema anaona wanakwenda kinyume na inavyotakiwa kufanyika.
“Viongozi
wa sasa wanaonekana hawajali misingi ya maadili kwa sababu jamii yetu
yenyewe imeonyesha kutochukizwa na suala hili la mmomonyoko wa maadili
na wala jamii haijalipa uzito unaostahili,” alisema Jaji Warioba wakati
wa uzinduzi wa kampeni ya Vuguvugu la uhuishaji wa Maadili kwa Jamii
(Moral Rivival Movement).