Saturday, September 5, 2015

Putin: Sera mbovu za Ulaya, sababu ya mgogoro wa wahajiri'


 
Rais Vladmir Putin wa Russia amesema leo kuwa, mgogoro wa wahajiri unaolikabili bara Ulaya kwa sasa umetokana na sera mbovu za kigeni za nchi za bara hilo hususan zile ambazo ni wanachama wa Umoja wa Ulaya (EU). Kiongozi huyo amesisitiza kuwa, uingiliaji wa Wamagharibi katika mambo ya ndani nchi za Mashariki ya Kati na kaskazini mwa Afrika ni moja ya sababu za kuibuka mgogoro wa wahajiri katika nchi za EU.

Rais Putin amesema viongozi wa Ulaya wameingia kwenye mtego wa Marekani kwa kukubali kufuata kibubusa sera zake hususan katika ulimwengu wa Kiislamu na kwa mantiki hiyo migogoro ya kisiasa katika nchi za Syria, Libya, Somalia, Yemen na kwingineko imewafanya raia wa nchi hizo kukimbilia usalama wao barani Ulaya. "Wanawatwisha watu sera zao kwa lazima bila ya kujali itikadi zao za kidini, utamaduni wao na muundo wa jamii. Hilo lazima litaleta matatizo makubwa", amesema kiongozi huyo. Rais wa Russia ametahadharisha kuwa, EU na Marekani zisipobadili sera zao za kigeni mgogoro huo utakuwa mpana zaidi katika siku za usoni.
SOURCE: TEHRAN

0 comments:

Post a Comment